Site icon A24TV News

Wafanyabiashara wadogo Tanzania na Kenya waeleza manufaa ya mradi wa barabara Tanga-Horohoro , wataka kuondolewa vikwazo mipakani.

mwandishi wetu,Tanga

Wafanyabiashara wadogo katika mpaka wa Tanzania na Kenya, eneo la Horohoro na Lungalunga ,wametaka serikali za Tanzania na Kenya, kuondoa vikwazo vya kibiashara ,hasa baada ya kukamilika miundombinu ikiwepo barabara ya Tanga- Horororo.

Barabara la lami ya Tanga- Horohoro, imejengwa na Serikali ya Marekani kupitia miradi ya malengo ya milenia(MCC).

Wakizungumza na mwandishi habari hizi, katika mpaka huo, baadhi ya wafanyabiashara wadogo wa Kenya na Tanzania, walitaka serikali za Kenya na Tanzania, kuendelea kupunguza vikwazo ili biashara iwe rahisi zaidi baina ya nchi moja hadi nyingine, hasa ya mazao, mifugo na bidhaa za ndani.

Joseph Mwanganya mfanyabishara mdogo wa Kenya kaunti ya Lungalunga ,alisema licha ya serikali za Afrika Mashariki kuwa na miundombinu bora mipakani lakini, bado changamoto kuwa ni vikwazo vya kibiashara.

“sisi kama wafanyabiashara tunataka uhuru wa kufanya biashara hasa hizi ndogondogo turuhusiwe kuingia katika nchi hizi mipakani na kupitisha biashara ndogondogo hasa hizi za mazao”alisema

Mwenyekiti wa Kitongoji cha Duga Maforoni, Horohoro, Tanzania, Zahoro Juma, alisema kwa sasa upande wa Tanzania biashara zimeimarika sana kutokana na uwepo wa barabara nzuri ambayo inarahisisha usafirishwaji wa bidhaa mbali mbali.

“kuna vikwazo vidogovidogo vya kiforodha lakini.,kubwa biashara zinakwenda vizuri hivi sasa kutoka Tanga hadi Horororo unatumia saa moja tofauti na miaka ya nyuma tulikuwa tunatumia saa sita kwa kilomita 65 tu”alisema

Mkuu wa mkoa wa Tanga, Omary Mgumba akizungumza na wananchi alisema serikali inajitahidi kupunguza vikwazo kwa wafanyabiashara wadogo katika mpaka huo na biashara zimeimarika sana tofauti na miaka ya nyuma.

“wafanyabiashara wadogo tunawaruhusu kufanyabiashara kilometa 10 ndani ya Tanzania na Kenya bila vikwazo“alisema.

Alisema hivi Sasa miundombinu imeimarika hasa barabara hivyo ni fursa kwa wafanyabiashara wadogo kuitumia na Serikali imetenga maeneo ya uwekezaji,ikiwepo maeneo ya viwanda na masoko ya bidhaa mbalimbali ikiwepo mifugo.

MWISHO.