Site icon A24TV News

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA ATANGAZA NEEMA KWA VIWANDA VIKUBWA NCHINI

Na Mwadishi wa A24Tv

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe. Dkt Ashatu Kijaji ( Mb.) amesema Serikali inafanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha viwanda vya nguo nchini vinavyoajiri watu wengi hususani wanawake na vijana vinafanya kazi kwa ufanisi ili kuongeza ajira, pato la taifa, kukuza biashara ya ndani na nje ya nchi na uchumi kwa ujumla.

Dkt. Kijaji ameyasema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha nguo cha A TO Z Bw. Kalpesh Shah akiwa na Meneja Mauzo ya Nje wa Kiwanda hicho Bw. Sylvester Kazi Oktoba 10, 2022 katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es salaam kwa lengo la kujadili na kitatua changamoto zinazoikabili sekta ya nguo nchini.

Aidha, katika kuendeleza sekta hiyo, Dkt. Kijaji amesema Serikaki inaendelea kuweka mazingira bora na wezeshi ili kuhakikisha pamba inayozalishwa nchini inakuwa na ubora unaotakiwa na inatosheleza mahitaji ya viwanda vya nguo nchini kwa mwaka mzima ili viweze kufanya kazi kwa ufanisi.

Dkt. Kijaji pia amesema ni muhimu kuanzisha viwanda vya kuchakata pamba (Spinning) nchini ili kuongeza thamani katika zao la pamba na kupunguza uuzaji wa pamba ghafi ambayo asilimia 70 ya pamba inayozalishwa nchini huuzwa nje ya nchi kama malighafi.