Site icon A24TV News

MAANDAMANO YA KUHAMASISHA SENSA ARUSHA YAFANA ,TAASISI YA KIDINI YA TWARIQATUL QADIRIYA JAILANIYA ARRAZAQIYA YAPONGEZWA

Na Joseph Ngilisho, ARUSHA

MAMIA ya wakazi wa jiji la Arusha wamejitokeza kwa wingi kushiriki maandamano makubwa ya kuhamasisha zoezi la sensa ya watu na makazi yaliyoandaliwa naTaasisi ya dini ya kiislamu ya Twarika Qadiriya mkoani Arusha ambapo wananchi hao walisema wapo tayari kuhesabiwa.

maandamano ya sensa na makazi jijini Arusha

Akiongea mara baada ya kupokea ujumbe wa maandamano hayo ,kamishna wa ardhi Mkoa wa Arusha,Essay Mwakatumbula aliwataka wananchi hao kuwa mabalozi wazuri wa kuhamasisha zoezi la Sensa ili kila mtu ashiriki kikamilifu zoezi hilo.

Aidha aliwataka wakazi wa jiji la Arusha kutoa ushirikiano wa dhati kwa makarani wa Sensa ikiwemo kutowaficha wenye ulemavu ili kuiwezesha serikali kuwatambua ili kuwapatia fursa mbalimbali.

Mwakatumbula ambaye alimwakilisha waziri wa Ardhi,nyumba na maendeleo ya makazi, Angeline Mabula, alisema ofisi yake itaendelea kushirikiana na taasisi hiyo ya dini katika kufanikisha zoezi la serikali la uhesabuji wa watu na makazi lenye lengo la kuirahisishia serikali katika kupanga mipango ya maendeleo.

Katika hatua nyingine Mwakatumbula alisema kuwa waziri Mabula amepokea ombi la taasisi ya Twarika kuhusu mpango wake wa kupata eneo lenye ukubwa wa ekari 10 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya mama na mtoto,ambapo waziri aliahidi kuchangia .

Kwa upande wake katibu wa taasisi hiyo ya kidini ya Twarika, mkoani hapa,Sheikh Haruna Husein alisema kuwa lengo la maandamano hayo ni kuhamasisha zoezi la Sensa ya watu na makazi inayotarajia kufanyika nchini nzima Agosti 23,mwaka huu.

Alisema maandamano hayo ambayo yalishirikisha vikundi mbalimbali vya maendeleo,wanasiasa, waendesha pikipiki,wazee wa ukoo na wananchi yalizunguka katika mitaaa mbalimbali ya jiji la Arusha huku yakichagizwa na vikundi vya ngoma na sarakasi .

“Tunawapongeza sana wananchi waliohamasika kushiriki maandamano haya ya kuhamasisha zoezi la Sensa, sisi kama taasisi ya dini tumefarijika sana kuona wananchi wameielewa serikali yao”alisema.

Wananchi walioshiriki maandamano hayo waliipongeza taasisi hiyo ya kidini kwa kuwa mstari wa mbele kuhamasisha mara kwa mara watu kujitoleza kuhesabiwa na walidai kuwa wapo tayari kuhesabiwa .

Ends..