Site icon A24TV News

MAHAKAMA YAMTAKA MWENYEKITI KADOGOO KUMLIPA FIDIA MILLION 250 MKUU WA MKOA STAAFU SANARE KWA LUGHA CHAFU ZA KUMZALILISHA

Arusha

Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha  imemwamuru Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli,Isack Joseph maarufu kwa jina la Kadogoo kumlipa shilingi milioni 250 Mkuu wa Mkoa Mstaafu,Loota Sanare kwa kumkashfu,kumdhalilisha na kumchafua kwa jamii kwa kumwita mwizi.

Uamuzi huo ulitolewa na Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha Aisha Ndosi baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote na kujilidhisha pasipokuwa na shaka yoyote kuwa Joseph alitamka maneno ya kashfa dhidi ya Sanare aliyewahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro.

Ndosi katika hukumu yake alisema kuwa utetezi uliotolewa na Joseph hakuwa na nguvu kwani ushahidi uliosikilizwa toka kwa mlalamikaji ulikuwa na mashiko na mahakama kumkuta na hatia ya kutoa maneno ya kuudhi na udhalilishaji dhidi ya Sanare.

Alisema baada ya kukutwa na hatia mahakama imemwamuru,Joseph kumlipa Sanare kiasi cha shilingi milioni 200 kwa kumchafua kwa jamii na pia imeamuriwa kumlipa shilingi milioni 50 kwa kumwita mwizi na mahakama imeamuru kuhakikisha Joseph analipa gharama zote za kesi hiyo toka ilipoanza hadi kwisha.

Naye Wakili wa Sanare,Kalimprit Mgalula baada ya hukumu alisema kuwa kwanza ameishukuru mahakama hiyo kwa kutenda haki na kuwataka wananchi wengine kuacha kutumia lugha za kuudhi ,kudhalilisha ,kuchafua pindi wanapopewa madaraka ya kiserikali na chama.

Wakili Mgadula alisema kuwa mteja wake Sanare ni mtu mwenye heshima zake kwa jamii ameshika nyadhifa mbalimbali serikalini na Chama Cha Mapinduzi{CCM} ngazi ya wilaya,Mkoa na Taifa,Sanare ni kiongozi wa mila wa jamii ya kifugaji ya Kimasai Laigwanani na Sanare ni mfanyabiashara maarufu Mkoani Arusha na anamiliki shule Monduli hivyo anastahili kuheshimiwa.

Alisema kumzungumzia Sanare kuwa ni mwizi,mpora ardhi na maneno mengi ya hovyo hovyo ya mtaani ni kumvua nguo kwa jamii ili aonekane hafai ni kosa hivyo mahakama imeona sahihi kwa kumwamuru mwenyekiti huyo kumlipa fidia Sanare ya shilingi miloni 250 na kulipa gharama za kesi.

Naye Sanare alisema kuwa kwanza ameishukuru Mahakama kwa kutenda haki jambo hili kwa kuona nilidhalilishwa nilifedheheshwa na kuomba viongozi walipewa madaraka kutumia lugha nzuri kwa jamiikwani madaraka waliyonayo ni ya muda tu.

Sanare alisema yeye ni kiongozi wa Milla ameitwa mwizi,ameitwa mpora ardhi kwa jamii hii imemdhalilisha na kumfedhehesha kwa jamii wakati eneo linalodaiwa ana hati iliyotolewa na serikali hivyo kuitwa mwizi na mpora ardhi ni kauli iliyomfedhehesha sana.

Alisema asingefika mahakamani kama angetii wito wa viongozi wa Milla,Serikali na chama waliomwita zaidi ya mara tatu lakini alikaidi kwa dharau na yeye kuamua kutafuta haki ya kusafishwa mahakamani na ameshukuru Mahakama imetenda haki yake.

Sanare alisema kashfa alizopewa na Joseph na kutaka gharama zote za fidia alizohitaji Mahakama imekubaliana nazo na amemtaka Joseph kuhakikisha anamlipa fedha hizo haraka iwezekanavyo kwani hatakuwa na msalie mtu tena kwani alimpa muda wa kuwomba radhi lakini alikaidi kwa kuwa ni kiongozi wa Halmashauri.

Joseph hakuwa tayari kuongea baada ya hukumu hiyo na kuondoka kwa kasi na gari yake huku akisema kuwa hana nafasi ya kuongea hadi awasiliane na mawakili wake.

Mwisho