Site icon A24TV News

CRDB RASMI YAKABITHIWA CHETI CHA KUTOA HUDUMA YA BIMA KWA WANACHI

Na Geofey Stephen Arusha

Kamishna wa bima nchini Dkt Baghayo Saqware amekabidhi cheti cha utoaji wa huduma ya bima kwa Benki ya CRDB ikiwa ni benki ya kwanza hapa nchini kupata cheti hicho kama kampuni tanzu kuanzisha huduma hiyo .

Akikabithi cheti hicho ,Kamishna Dkt Saqware amesema kuwa, anataka kuona benki hiyo inafanya kazi katika ubunifu wa hali ya juu na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ikilinganishwa na Taasisi zingine ambazo zimekuwa zikifanya kazi kwa mazoea.

Aidha amesema kuwa, kitendo cha benki hiyo kukidhi vigezo na kukabithiwa cheti hicho ni mfano wa kuigwa na taasisi zingine kwani uwepo wa bima hiyo utasaidia sana kutoa huduma za bima kwa wanachama wake na kukuza Pato la taifa

Amesema kuwa,hapo awali walikuwa wakitoa huduma hiyo kama mawakala/madalali lakini kwa sasa itakuwa ikitoa huduma hiyo rasmi kama kampuni ya Bima ya CRDB nchini.

Amefafanua kuwa ,matarajio ni kuona kuwa benki ya CRDB inatoa mchango mkubwa kwenye sekta ya bima kwani hadi sasa sekta ya bima imekuwa ikichangia pato la Taifa kwa asilimi moja ambayo ni ndogo sana na matarajio ni kufikia asilimia tatu.

“Ni matumaini yangu baada ya kuwa kampuni rasmi ya utoaji wa bima ningependa kuona mnahamasisha Watanzania pamoja na kuwapa elimu juu ya matumizi ya Bima kwani mpaka sasa watanzania wengi hawana uelewa wa kutosha juu ya maswala hayo.”amesema.

Aidha amesema kuwa, benki ambayo inatoa huduma zake kimataifa ikiwemo nchi ya Congo,Burundi,na Tanzania ni vizuri ubunifu uliotumika katika nchi hizo utumike kukuza sekta hiyo ya bima .

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela amesema kuwa, amefurahishwa sana kupata cheti hicho kama benki ya kwanza hapa nchini.

Nsekela amesema kuwa,mbali na kuanza kama mawakala wanajivunia kuona wamekuwa kampuni rasmi ya kutoa huduma ya Bima ambapo amesema wao watajiongeza kuhakikisha wanafikia makundi yote maalumu.

Aidha ametaja makampuni ambayo yatanufaika ni pamoja na wasafarishaji,wakulima ,wafugaji, viwanda ,ambapo huduma hizo zitakuwa zinatolewa kwa njia ya kidigitali ili kufikia walengwa waliokusudiwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa bima (CRDB ),Wilson Mzava amesema kuwa,CRDB imejipanga kuwahudumia watanzania wote na wategemee utofauti mkubwa endapo kutajitokeza majanga ya aina yoyote na matarajio ya kampuni hiyo ni kulipa fidia kwa haraka zaidi .

Aidha ameongeza kuwa, watanzania kuanzia sasa watarajie kuwepo kwa huduma hiyo katika matawi ya benki ya CRDB pamoja na mawakala kwa ajili ya kupata huduma hiyo ambayo inapatikana nchi nzima.

Mwisho.