Site icon A24TV News

MONGELA NA VIONGOZI WA CCM MKOA WA ARUSHA WAMPONGEZA MFANYA BIASHARA KWA KUJALI MAENDELEO

Na Geofrey Stephen Arusha

VIONGOZI mbalimbali wa dini, Chama na serikali Mkoa wa Arusha, wamemwagia sifa FANYABIASHARA Maarufu wa Madini jijini Arusha,Faisal Shahbhai wakidai ni mfano wa kuigwa ,mwenye moyo wa kizalendo kutokana na jitihada zake za kupigania maendeleo ya mkoa pamoja na kuwaunganisha wafanyabiashara wadogo na serikali yao .

Akiongea katika hafla ya chakula cha jioni kwa ajili ya kufuturisha waislamu ,kilicho andaliwa na mfanyabiashara huyo kwa kushirikiana na chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha ,mkuu wa mkoa huo, John Mongella alidai kuwa Mkoa unajivunia kuwa na wafanyabiashara wazalendo wenye kupenda maendeleo ya Taifa Lao.

Mkuu huyo wa mkoa alisema Faisal amekuwa ni mtu mwenye ushirikiano mkubwa na jamii pamoja na serikali ya mkoa na amekuwa mstari wa mbele kushiriki shughuli za maendeleo.

“Mimi ni kati ya watu ambao ninabahati ya kufahamiana na Faisal ni mtu wa ibada sana ,nafikiri ni mfano wa kuigwa sio kwamba anauwezo sana wa kifedha ni mungu amemjalia kuwa na moyo wa kujitolea “

Alitoa rai kwa wafanyabiashara wengine kuiga mfano huo huku akisisitiza kwa viongozi wa dini kuliombea Taifa pamoja na kuuombea mkoa wa Arusha ili uendelee kuwa na utulifu na mshikamano .

Awali Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha ,Zelothe Steven, alimtaja Faisal kama mfanyabiashara mwenye upendo na maoni mwenye nia thabiti ya kushirikiana na jamii na mkoa wa ARUSHA .

Alisisitiza kuwa katika mpango wa maendeleo wa taifa lazima wafanyabiashara waheshimiwe na wasibughudhiwe jambo litakalosaidia kuinua uchumi wa nchi .

“Mimi kama mwenyekiti wa ccm sipendi wafanyakazi wabughudhiwe napenda kuona watu wote wanaheshimiwa napenda kuona haki inatendeka”

Naye mwenyekiti wa wafanyabiashara wadogo wa madini (BLOKES)Mkoa wa Arusha, Jeremia Simon, alisema kuwa Faisal amekuwa kiungo kikubwa cha wafanyabiashara wadogo wa madini na serikali yao.

“Faisal amekuwa akisaidia makundi mbalimbali ya wajasiriamali na aliwahi kuwalipia leseni wachuuzi 100 wa madini na kila leseni ilikuwa ni sh,250,000 ambao walikuwa wakibughudhiwa kwa kufukuzwa na kuwekwa mahabusu kwa kufanya biashara bila leseni”

Kwa upande wake katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mussa Matoroka alimshukuru mfanyabiashara huyo kwa kufanikisha suala la kuandaa chakula cha jioni kwa ajili ya waislamu waliofunga na kuyashirikisha makundi ya bodaboda,bajaji na akina mama.

Sheikh wa mkoa wa Arusha,Shaaban bin Juma alisema jambo lililofanywa na Faisal kutoa chakula kwa jamii katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu ni tendo la kafara kwa maana kwamba ukifanikiwa unaondolewa dhambi,misukosuko na lolote baya ulilonalo ama linalokwijia.

“Tendo hili lililofanywa na Faisal ni mfano mzuri wa kuigwa kwa waislamu na wasio waislamu kwani hutapungukiwa na chochote”

Awali mfanyabiashara Faisal,aliishukuru serikali chini ya chama cha Mapinduzi kwa kufanikisha maandalizi ya chakula cha jioni kwa ajili ya waislamu waliofunga katika mwezi mtukufu wa ramadhani

“Ninachoweza kufanya ni mungu kunijalia kuwa na roho hiyo naishukuru sana serikali na chama cha Mapinduzi kwa kutujalia uhuru huu na kufanikisha jambo hiki” .

Ends…..