Site icon A24TV News

Tanzania na China Kuendeleza Uhusiano wa Kibiashara

Na Mwandishi wa A24Tv .

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya watu wa China zimeahidi kuendeleza uhusiano wa kibiashara baina ya nchi hizo kwa kuzingatia misingi ya uhusiano na ushirikiano wa kirafiki uliokuwepo tangu mwaka 1961 ili kuenzi mazuri yaliyofanywa na waasisi wa nchi zote mbili walioanzisha uhusiano huo.

Hayo yalisemwa na Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji(Mb.)
alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa China nchini, Mhe. Chen Mingjian katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam Februari 23, 2023

Dkt. Kijaji alisema Tanzania iko tayali kuendeleza uhusiano huo ili kuwawezesha wafanyabiashara wa pande zote mbili kushirikiana na kufanya biashara zao ili kuongeza ajira na kukuza uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.

Aidha, Waziri Kijaji pamoja na Balozi huyo walijadiliana kuhusu namna ya kuenzi reli ya TAZARA na kufufua Kiwanda cha Urafiki ambacho ni matunda ya uhusiano baina ya nchi hizo pamoja na mikakati mbalimbali ya kuendeleza biashara

Naye Balozi wa China nchini, Mhe. Mingjian amesema kuwa Serikali yake wakati wote imekuwa rafiki mzuri kwa Serikali ya Tanzania na uhusiano wa kibiashara ni mzuri na kwa sasa China inapokea parachichi ya Tanzania na iko tayari kupokea mazao mengine hususani maharage ya soya