Site icon A24TV News

VURUGU ZAIBUKA MSIBA WA MATAJIRI ARUSHA,MWANDISHI WA AYOTV ANYANG’ANYWA CAMERA

Mwandishi wa A24Tv Arusha .

Katika hali isiyo ya kawaida vurugu zimeibuka katika msiba wa watoto wawili wa matajiri jijini Arusha ambao walikuwa ni wachumba waliofariki ajalini baada ya mwandishi wa habari kutoka AyoTV kunyang’anywa camera.

Mbali na kunyang’anywa camera mwandishi huyo alinyang’anywa kadi na kisha kuvunjwa na ndugu wa karibu akiwemo mdogo wa marehemu,Brighton Temu maarufu kama “Bonge “.

Vurugu hizo zimefuatia mara baada ya mwandishi huyo,Gedfrey Thomas kutinga msiba
ni kwa marehemu, eneo la KwaMrefu majira ya saa 10:30 leo jioni kufuatilia tukio la kifo cha mtoto wa Tajiri Denso.

Taarifa zimeeleza kwamba mara baada ya mwandishi huyo kutinga msibani hapo akiwa ameshikilia camera yake mkononi ndipo kundi la vijana waliojitambulisha ndugu wa karibu akiwemo mtoto wa mfanyabiashara anayemiliki mgahawa wa Uzunguni City Park ,Kevin Masuwa alimvamia na kutishia kumpiga mwandishi huyo.

Taarifa kutoka msibani zimeeleza kuwa kundi hilo la vijana wanaodaiwa kuwa katika hali ya ulevi ndipo lilimuamuru mwandishi huyo akabidhi camera na baada ya kuwakabidhi walichomoa kadi na kisha kuivunja na kisha wakamrejeshea camera yake.

Hatahivyo,taarifa zimedai kuwa mara baada ya vurugu hizo ndipo baba wa marehemu tajiri Temu maaarufu kama “Denso “ndipo alipomfuata mwandishi huyo na kumuuliza gharama za kadi hiyo ili amlipe lakini mwandishi huyo alikataa na kudai anahitaji kadi pekee.

Akihojiwa na waandishi wa habari Mwandishi huyo kwanza alilaani tukio hilo na kudai anawatambua vijana waliomfanyia fujo na kumyang’anya vifaa vyake vya kazi.

Mwandishi huyo alisema kwamba yeye alifika msibani hapo kufuatilia tukio la ajali lililopekea mauti ya kijana huyo kama Mwandishi na ghafla alipoingia ndani ya eneo la tukio alishangaa kuvamiwa na kundi la vijana mbalimbali.

“Mimi baada ya kufika msibani niliingia moja kwa moja eneo la tukio nikiwa nasogea ndani ghafla walitokea vijana ninaowatambua kwa sura wakaniamuru niwakabidhi camera nilipotaka kukataa walitishia kunipiga ndipo nikawakabidhi wakachomoa kadi na kisha kuivunja “alisema Mwandishi huyo

Hatahivyo,alisisitiza kuwa kitendo kilichofanyika sio cha uungwana na anajiandaa kutoa taarifa mbele ya jeshi la polisi mkoani Arusha.

WATOTO wawili wa Matajiri wakubwa katika jiji la Arusha,wanaodaiwa kuwa ni wachumba , Estomi Temu na mpenzi wake Nice Mawala(24)Mkazi wa Njiro walifariki dunia jana kwa ajali mbaya eneo la kwa Mrefu katika jiji la Arusha .

Kwa mujibu wa shuhuda wa tukio hilo ,ajali hiyo iliyotokea majira ya saa 7 usiku katika eneo hilo wakati gari la kifahari walilokuwa wakitumia lilikuwa kwenye mwendo kasi.

Katika tukio hilo linalodaiwa walitoka Klabu ,Nice alipasuka kifua na kuvunjika mkono wa kulia huku Estomi akiumia kwa ndani na kuvuja damu masikioni puani na mdomoni.

Mwisho.