Site icon A24TV News

Hospitali ya Mt.Elizabeth yajipanga kuboresha miundo mbinu

Arusha.Hospitali ya Mtakatifu Elizabeth (kwa pandre Babu) Ngarenaro wamejipanga kuboresha miundombinu katika hospitali hiyo kwa kujenga jengo la ghorofa nne ili kuweza kuhudumia wananchi wengi zaidi kulingana na uhitaji mkubwa uliopo.

Hayo yalisemwa Jijini Arusha na Mganga Mkuu wa hospital hiyo, Dokta Rohela Kaseriani wakati akizungumzia mikakati mbalimbali katika kuboresha hospitali hiyo ili iweze kuhudumia wananchi wengi zaidi na kutoa huduma mbalimbali za muhimu ambazo hazikuwepo.

Alisema kuwa ,hospitali hiyo ambayo ilianza mwaka 1974 Kama zahanati, 1984 ilipandishwa daraja na kuwa hosptali ambapo mwaka 2011 iliteuliwa na kuwa hospitali teule ya Jiji la Arusha,huku ikitoa huduma zote kama hospitali teule  ya Jiji.

Alisema kuwa,Hospital hiyo  imekuwa ikitoa huduma mbalimbali za wagonjwa wa nje na wagonjwa wa kulazwa pia zimo kiliniki za madaktari bingwa wa macho(opthamologist), Watoto (Peadritician), magonjwa yasiyo ya upasuaji – Internal medicine (Physcian) magonjwa pua ,masikio na koo(ENT),

Ambapo wanatoa pia huduma zingine ikiwemo ya Magonjwa ya Ngozi(Dermatologist)matatizo ya njia za mkojo(urologist), wakina mama(Gynaclogist),mifupa(Orthopedic)na huduma za upasuaji(surgery).Pia vipo vipimo vya maabara,X ray,Ultra sound,ECHO,ECG.

“kanisa lipo kwenye  mchakato wa kuanza ujenzi mkubwa wa hospitali hiyo ambapo wamejipanga kujenga  jengo hilo la ghorofa kwa awamu, ambapo awamu ya kwanza wataanza na jengo la wagonjwa wa nje ambalo litawezesha kuhudumia wananchi wengi  zaidi na kuweza kutoa huduma bora mbalimbali ambazo hazikuwepo ikiwemo chumba cha uangalizi maalumu wa wagonjwa(ICU),chumba cha upasuaji cha kisasa(theatre),eneo la wagonjwa wa dharura(emergencymedicine), machine za CT scan,MRI, mashine ya kutengeneza oxygen(Oxygen plant), huduma ya watoto njiti kwani sasa hivi wamekuwa wakiwahamishia hospitali ya Mount Meru na ALMC, pia kuboresha maabara  “alisema Dokta Rohela.

Dokta alisema kuwa,pamoja na huduma mbalimbali ambazo zimekuwa zikitolewa na hospitali hiyo,pia wamekuwa wakishirikiana na serikali kuhakikisha kuwa huduma za wazee, watoto, wanawake wajawazito,na makundi maalumu wanazitoa bure kwa kuzingatia miongozo ya serikali.

Alisema  kuwa,wakishaboresha hospitali hiyo wana matarajio kuomba kibali cha kuwa hospital ya rufaa hatua ambayo itawawezesha kutoa huduma bora zaidi za kibingwa na kibobezi  kwa wanachi wa Jiji la Arusha na nje ya Jiji la Arusha.

Mwisho.